Thursday, November 8, 2012

STRAIKA JELA MIAKA SABA KWA KUKUTWA NA UNGA

Michael Branch alivyokuwa kipindi akicheza soka

Mshambuliaji wa zamani wa klabu ya Everton Michael Branch amekutwa na hatia na kufungwa jela miaka saba (7) kwa kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya. Michael pichani ambaye pia amewahi kuzichezea klabu za Manchester City, Wolves na Reading alitiwa mbaroni na polisi wa jiji la Liverpool kabla ya kufikishwa mahakamani kwa makosa mawili ambapo alikiri yote kabla ya kupewa hukumu hiyo.
Branch, 34 alikiri kuuza karibu kilo 3 za amphetamine kwa mtu mmoja katika maegesho ya magari jijini Liverpool na pia polisi walimkuta na kilo 1 ya cocaine ambayo inakisiwa kuwa na thamani kati ya pauni 40,000 hadi 50,000 alipopekuliwa nyumbani kwake Merseyside mapema mwezi Julai mwaka huu.
Akihojiwa na Livepool Echo, msemaji wa The Serious Organised Crime Agency amesema hili ni tukio kubwa kuwahi kufanywa na mtu ambaye awali alikuwa ni kioo cha jamii (mtu wa mfano wa kuigwa). Msemaji huyo pia aliwaasa watu kuwa, kujihusisha na biashara ya madawa ya kulevya na mihadarati ni tendo lililo kinyume cha sheria na mwisho wake ni kifungo na kamwe haliwezi kumfanya mtu kuwa tajiri au kuishi katika maisha ya umaarufu.
Branch atakumbukwa kuwa mmoja kati ya wachezaji waliovumbuliwa na kuendelezwa na shule ya mpira ya klabu ya Everton ambaye kwa kipaji chake alipata nafasi kwenye timu ya wakubwa ya Everton ( maarufu kama The Toffees ) alipofikisha umri wa miaka 17 ambapo hadi anafika umri wa miaka 20 alifanikiwa kuifungia Everton mabao 3. Wakati huo watu wengi walimtazamia kuja kuwa mmoja wa mmoja kati ya wachezaji tegemeo wa klabu hiyo kwa siku za usoni lakini ndoto hizo zilipotea pale aliyekuwa meneja wa timu hiyo Joe Royle alipoondoka klabuni hapo. Baada ya hapo Branch alianza kupigwa danadana kwa kuhamishwa kwa mkopo kwenda Manchester City, Birmingham, na Wolves kabla ya kuuzwa kwa timu ya Molineux mnamo mwaka 2000 kwa ada ya pauni 500,000.
Katika kipindi chake alifanikiwa kufunga mabao sita (6) tu katika mechi 67 alizocheza katika ligi akiwa Molineux na baadae alikopeshwa kwa klabu za Reading, Hull, Bradford, na Chester. Alipofikisha umri wa miaka 28 aliachana na mpira wa ushindani na kujiunga na klabu za Halifax na Burscough ambazo hazishiriki ligi.

No comments:

Post a Comment